Takwimu za Bolt: Zaidi ya Asilimia 70 ya Watanzania Wachagua Huduma za Usafiri Nafuu Kadri Mahitaji ya Huduma za Gharama Kubwa Yanavyopungua
Dar es Salaam, 20 Agosti 2026
Takwimu mpya za Bolt Tanzania zinaonesha kuwa gharama nafuu zimeendelea kuwa kigezo kikuu kinachoongoza maamuzi ya Watanzania wanapotumia huduma za usafiri wa mtandao, ambapo zaidi ya asilimia 70 ya safari zote sasa hufanyika kupitia huduma za Bajaji na Bodaboda, huku mahitaji ya huduma za magari ya gharama kubwa yakianza kupungua.
Mabadiliko hayo yanakuja miezi michache baada ya Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri Ardhini (LATRA) kufanya marekebisho ya viwango vya chini vya nauli kufuatia ongezeko la asilimia 33.4 la bei za mafuta, hatua iliyosababisha kupanda kwa nauli katika makundi yote ya huduma za usafiri wa mtandao. Ingawa lengo la marekebisho hayo lilikuwa kulinda kipato cha madereva, pia yaliongeza tofauti ya bei kati ya huduma za kawaida na zile za gharama kubwa, hali iliyowafanya abiria wengi kuelekea kwenye chaguo nafuu zaidi.
Kwa mujibu wa Bolt, makundi ya magari ya gharama kubwa kama Standard na XL yamekuwa yakirekodi ukuaji mdogo wa mahitaji katika miezi ya karibuni, huku watumiaji wengi wakihamia kwenye huduma zenye gharama nafuu kwa safari zao za kila siku.
Akizungumzia mwenendo huo, Meneja Mkuu Mwandamizi wa Bolt Afrika Mashariki, Dimmy Kanyankole, alisema takwimu hizo zinaakisi mabadiliko ya vipaumbele vya watumiaji, badala ya kupungua kwa matumizi ya huduma za usafiri wa mtandao.
"Marekebisho ya hivi karibuni ya nauli yamebadili namna watu wengi wanavyofikiria kuhusu usafiri wa kila siku. Watanzania bado wanathamini urahisi na usalama wa huduma hizi, lakini kwa sasa gharama nafuu imekuwa kigezo muhimu zaidi.
Tunachokiona si kupungua kwa matumizi ya ride-hailing, bali ni ongezeko la abiria wanaochagua huduma inayolingana na uwezo wao wa kifedha."
Aliongeza kuwa uwepo wa makundi mbalimbali ya huduma unawawezesha abiria kufanya maamuzi yanayozingatia uwezo wao wa kifedha, huku ukiendelea kuhakikisha madereva wanapata kipato endelevu ndani ya mfumo wa sasa wa kanuni za sekta.
Bolt imesema mwenendo huo unaonesha umuhimu wa kuendelea kuwa na mfumo mpana wa huduma za usafiri wa mtandao unaotoa chaguo mbalimbali kulingana na mahitaji ya wateja. Kadri gharama za usafiri zinavyoendelea kubadilika, kampuni hiyo imesisitiza dhamira yake ya kuendelea kupanua huduma nafuu za usafiri bila kuathiri ubora, usalama na uaminifu wa huduma zake.

Hakuna maoni: