SERIKALI YAPOKEA MAPENDEKEZO YA KUWAINUA WACHIMBAJI WADOGO KIUCHUMI

Na Mwandishi Wetu, 

Dar es Salaam.

Serikali imepokea mapendekezo ya wataalamu yaliyolenga kuweka mfumo madhubuti wa kuwawezesha wachimbaji wadogo wa madini nchini, huku ikiahidi kuyafanyia kazi kwa haraka ili kuongeza uzalishaji, ajira na mchango wa sekta ya madini katika uchumi wa taifa.

Akizungumza wakati wa hafla ya kupokea mapendekezo hayo jijini Dar es Salaam Juni 13, 2026, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, amesema kuwa upatikanaji wa mitaji, teknolojia za kisasa na taarifa sahihi za kijiolojia ni nguzo muhimu katika kuwawezesha wachimbaji wadogo na kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Amesema Serikali imejielekeza katika kutatua changamoto zinazokwamisha maendeleo ya wananchi, ikiwemo kuongeza mitaji, kuzalisha ajira na kupunguza umaskini, huku akieleza kuwa sekta ya madini ina nafasi kubwa katika kufanikisha malengo hayo.

Prof. Mkumbo ameongeza kuwa kuwawezesha wachimbaji wadogo kutasaidia kuongeza kipato cha wananchi na kuchochea maendeleo ya kiuchumi, akibainisha kuwa mikoa yenye shughuli nyingi za uchimbaji bado inakabiliwa na viwango vya umaskini vinavyohitaji hatua za makusudi.

Kwa upande wake, Waziri wa Madini Anthony Mavunde amesema mchango wa wachimbaji wadogo umeendelea kuimarika licha ya changamoto wanazokutana nazo, na kwamba kwa sasa wanachangia takribani asilimia 40 ya mapato ya sekta ya madini.

Amesema mageuzi yaliyofanywa katika sekta hiyo yameongeza makusanyo ya Serikali kutoka shilingi bilioni 161 mwaka 2015/16 hadi zaidi ya shilingi trilioni 1.3 kufikia Juni 13, 2026.

Mavunde amesema Serikali imeanza utekelezaji wa Kampuni ya Dhamana ya Mikopo (Credit Guarantee Corporation) itakayosaidia wachimbaji kupata mikopo kutoka taasisi za fedha, hatua inayolenga kupunguza changamoto ya mitaji inayowakabili.

Mwenyekiti wa Kamati ya Wataalamu, Dkt. Victor Tesha, amesema kamati imependekeza kuanzishwa kwa Mfuko wa Madini Tanzania utakaosaidia kugharamia miradi ya uchimbaji, ununuzi wa mitambo, tafiti na upatikanaji wa taarifa za kijiolojia.

Amesema hatua ya baadaye ni kuanzishwa kwa Benki ya Wachimbaji itakayotoa huduma za kifedha zinazozingatia mahitaji maalumu ya sekta ya madini.

Naye Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Wadogo Tanzania, John Bina, ameipongeza Serikali kwa kuendelea kusikiliza na kufanyia kazi changamoto za wachimbaji, akisema hatua ya kutenga asilimia 10 ya mapato ya madini kwa ajili ya utafiti itasaidia kukuza sekta hiyo na kuongeza tija kwa wachimbaji wadogo nchini.

Hakuna maoni:

Inaendeshwa na Blogger.